News

KWANDIKWA: ATEMA CHECHE KWA MKANDARASI KUONGEZA MITAMBO NA WAFANYAKAZI

Naibu Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano (Sekta ya Ujenzi), Mheshimiwa Elias Kwandikwa (Mb), ametoa muda wa siku 21 kwa Mkandarasi Nyanza Road Works kuongeza vifaa vya kazi na wafanyakazi ili kuongeza kasi ya ujenzi wa barabara ya Nyakanazi-Kibondo yenye urefu wa KM 50 inayojengwa kwa kiwango cha lami.

Mhe. Kwandikwa ametoa agizo hilo mkoani Kigoma leo, wakati akikagua maendeleo ya ujenzi wa mradi huo ambapo pamoja na mambo mengine amesisitiza kuwa ujenzi huo unatakiwa kukamilika haraka ili kuweza kufungua mkoa huo na kurahisha shughuli za usafirishaji.

"Hakikisheni ndani ya wiki tatu vifaa vya ujenzi vinakuwepo eneo la kazi na ajira zinatolewa kwa wananchi ili mradi ukamilike mapema iwezekanavyo", amesisitiza Mhe. Kwandikwa.

Kuhusu suala la malipo, Mhe. Kwandikwa amefafanua kuwa hivi sasa hakuna tatizo lolote la malipo kwani mkandarasi ameshalipwa na kilichobaki sasa ni mkandarasi kufanya kazi usiku na mchana ili ujenzi ukamilike.

"Tunamshukuru Mhe. Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa juhudi anazozifanya kwani hivi sasa hali ya fedha ni nzuri, mapato yanaongezeka hivyo tutegemee kupata matunda ya maendeleo ya miundombinu bora hapa nchini", amesema Naibu Waziri Mhe. Kwandikwa.

Aidha, Naibu Waziri amewataka makandarasi wazawa kuongeze juhudi kubwa katika miradi ya ujenzi hapa nchini hadi kufikia zaidi ya asilimia 60 ili waweze kupewa fursa za miradi mingi ya ujenzi wa barabara.

"Kazi za wazawa zikifanya vizuri na vijana wetu wakifanya kazi kwa uadilifu na uzalendo kutaongeza tija katika maendeleo ya miundombinu nchini na hatua nzuri ya kufikia katika uchumi wa kati", amesema Mhe. Kwandikwa.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kakonko Kanali Hosea Ndagalla, amesema kwa niaba ya wananchi wake wanaungojea mradi huo ukamilike kwa wakati na ubora ili kuondoa adha wanazozipata hasa vipindi vya mvua.

Naye Meneja wa Wakala wa Barabara (TANROADS), mkoa wa Kigoma Eng. Narcis Choma, amemuahidi Mhe. Kwandikwa, kuwa atamsimamia mkandarasi na kuhakikisha kasi ya ujenzi inaenda sambamba na vifaa pamoja na wafanyakazi.

Mkakati wa Serikali ya Awamu ya Tano ni kuhakikisha inaboresha miundombinu ya barabara katika ukanda wa magharibi ili kuiwezesha kufanya biashara kiurahisi na mikoa mingine ya Tanzania na nchi za Congo DRC, Rwanda na Burundi.