News

Serikali inajenga zaidi ya Kilometa 150 za BRT Dar es Salaam

 

Serikali inajenga zaidi ya Kilometa 150 za BRT Dar es Salaam

08 Desemba, 2023

SERIKALI kupitia Wakala ya Barabara Tanzania (TANROADS) inajenga zaidi ya Kilomita 150 za barabara za magari ya mwendo wa haraka BRT (Mwendokasi) katika Jijini la Dar-es Salaam.

Hayo yameelezwa katika mkutano wa 16 wa mapitio ya kujadili masuala ya uchukuzi unaofanyika kwenye Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Arusha (AICC) kuanzia tarehe 5-8 Desemba, 2023.

Akizungumza mbele ya Waziri wa Uchukuzi Prof. Makame Mbarawa aliyefungua Mkutano huo; Mkurugenzi wa Mipango ya Miundombinu, Mhandisi Ephatar Mlavi, amesema ujenzi huo wa BRT unatekelezwa kwa awamu sita, ambapo tayari awamu ya kwanza iliyohusisha barabara za kutoka katikati ya Jiji hadi Kimara umekamilika na huduma ya usafiri unafanywa na Wakala wa Mabasi yaendayo Haraka (UDART), na sasa imeongezwa hadi Mbezi na itafika hadi Kibaha.

Amesema awamu ya pili ni ya barabara ya kutoka katikati ya Jiji hadi Mbagala, ambayo nayo imekamilika kwa asilimia 99, na sasa wakandarasi wanamalizia kazi mbalimbali ikiwemo alama za barabarani; na baadaye itaendelezwa hadi Kongowe; huku awamu ya tatu ikitoka Gongolamboto hadi katikati ya Jiji, ambayo nayo imeshaanza kujengwa.


Amesema awamu ya nne itahusisha barabara kutoka katikati ya Jiji hadi Tegeta (DAWASA) pamoja na kipande cha kutoka Mwenge hadi Ubungo, na awamu ya tano itahusisha barabara ya Mandela kutoka Ubungo hadi Bandari, pamoja na kipande cha barabara ya Tabata kutoka Segerea hadi Kigogo.

“Awamu ya sita bado haujafanyiwa usanifu wa kina lakini inatarajiwa kuhusisha barabara ya Mwai Kibaki (Morocco hadi Kawe); Kimara hadi Kibamba; na Mbagala hadi Vikindu” amesema Mha. Mlavi.

Ameongeza kuwa kukamilika kwa barabara hizo zote kutasaidia kutatua changamoto ya msongamano wa magari katika njia kuu za Jiji la Dar es Salaam, na kuleta faida kwa magari makubwa yanayosafirisha mizigo kwenye nchi za Jirani, ambayo kimsingi ndio yenye kuchangia uchumi wa nchi na nchi Jirani kutembea kwa urahisi na kuleta faida ya kiuchumi