News

DARAJA LA JP MAGUFULI (KIGONGO-BUSISI) KUKUZA UCHUMI KANDA YA ZIWA

DARAJA LA JP MAGUFULI (KIGONGO-BUSISI) KUKUZA UCHUMI KANDA YA ZIWA

Mwanza

08 Juni, 2025

Waziri wa Ujenzi Abdallah Ulega, amesema ujenzi wa Daraja la J.P Magufuli (Kigongo - Busisi ) lenye urefu wa kilomita 3 utarahisisha huduma za usafiri na usafirishaji hivyo kukuza uchumi wa wananchi Kanda ya Ziwa.

Ulega amesema hayo mkoani Mwanza leo Juni 8, 2025 wakati akielezea Mafainikio katika Sekta ya Ujenzi kwa kipindi cha miaka minne ya uongozi wa Rais Dkt. Samia ambapo amesema daraja hilo lina uwezo wa kupitisha magari zaidi ya 20,000 kwa siku.

Ulega amebainisha kuwa wakati Mhe Rais Samia anaingia madarakani mwaka 2021 ujenzi wa daraja hilo ulikuwa umefikia asilimia 25 tu na sasa ujenzi huo umekamilika kwa asilimia 100.

Waziri Ulega ametaja mafanikio mengine yaliyofikiwa kuwa ni kuongezeka kwa mtandao wa barabara zinazohudumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) kutoka Kilometa 36,361.95 hadi kufikia Kilometa 37,435.04 kutokana na barabara hizo kupandishwa hadhi na kuwa za Kitaifa.

Aidha, amesema katika kipindi hicho cha miaka minne ya Serikali ya Awamu ya Sita barabara zenye urefu wa Kilometa 15,511.25 ziko katika hatua mbalimbali ya ujenzi.Ulega amesisitiza kuwa katika kurahisisha huduma za usafiri na uchukuzi, Serikali imekamilisha ujenzi wa madaraja makubwa nane (8) na mengine 12 yapo katika hatua mbalimbali za ujenzi nchini kote.

Kadhalika, Ulega amesema Serikali inaendelea na mkakati wa kupunguza msongamano wa magari katika miji mikubwa hapa nchini hususan Mikoa ya Dar es Salaam, Dodoma, Mwanza na Mbeya, ili kuhakikisha wafanyabiashara na wananchi wanafikia huduma kwa wakati na kupunguza gharama za uendeshaji wa magari kwa kukaa kwenye foleni kwa muda mrefu.

“Katika kujenga barabara tunaweka pia ulinzi wa barabara hizo kwa kujenga mizani zitakazosimamia udhibiti wa magari ikiwemo kufunga mizani za kisasa zenye matumizi madogo ya binadamu, kufunga mizani za kielektroniki zinazopima magari yakiwa kwenye mwendo na kufunga mfumo wa ufuatiliaji wa CCTV kamera katika vituo vyote vya mizani ifikapo 2027”, ameeleza Ulega.