News

RAIS SAMIA AWEKA REKODI YA UJENZI WA MIUNDOMBINU KIGOMA

RAIS SAMIA AWEKA REKODI YA UJENZI WA MIUNDOMBINU KIGOMA

Kigoma, 22 Julai, 2026

Waziri wa Ujenzi Abdallah Ulega ameeleza kuwa katika kipindi cha miaka mitano ya utawala wa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan umeufungua Mkoa wa Kigoma kwa kufanya ufikike kwa urahisi, kupunguza gharama za safari na kufungua fursa za kiuchumi kwa wakazi wake.

Akizungumza kwenye mikutano aliyofanya kwenye maeneo tofauti kukagua maendeleo ya ujenzi wa miradi inayoendelea Waziri Ulega, amesema Kigoma ya sasa ni tofauti kabisa na ile ilivyokuwa wakati Rais Samia akiingia madarakani mwaka 2021.

Akizungumza kwa kutumia takwimu, Ulega alitoa mfano wa mtandao wa barabara za lami ambao alisema kwa miaka takribani 60 ya Uhuru, Kigoma ilikuwa na kilomita za barabara 259 za lami, lakini serikali ya Rais Samia imejenga barabara kilomita 335 kwa Mkoa huo.

“Hii maana yake ni kwamba kwa miaka mitano tu, serikali ya Rais Samia imejenga kilomita za lami ambazo ni zaidi ya kilomita zilizokuwepo kabla yake kwa miaka 60.

“Matokeo yake leo Kigoma ina mtandao wa barabara za lami wenye urefu wa kilomita 594 ambayo ni ongezeko la zaidi ya asilimia 100 ya kiwango kilichokuwepo zamani,” alisema Ulega. 

Ulega ambaye yuko katika ziara ya kikazi mkoani Kigoma, alifanya ukaguzi wa takribani wilaya nne tofauti za Mkoa wa Kigoma ambapo viongozi, wabunge na wananchi wa mkoa huo walieleza tofauti zilizoanza baada ya mabadiliko hayo.

Akihutubia Kasulu, Ulega alisema kwa ujumla Serikali imetumia zaidi ya shilingi Bilioni 600 kwa ajili ya ujenzi wa miradi ya kimkakati tisa katika Mkoa wa Kigoma peke yake.

Waziri huyo alisema kinachoendelea Kigoma ndiyo taswira pia ya maendeleo makubwa ya ujenzi yanayoendelea katika mikoa tofauti nchini Tanzania kwa sababu Rais Samia anaamini barabara ni mlango wa fursa kwa walio wengi.

Akiwa Kigoma Vijijini, Ulega alipita katika barabara ya urefu wa km 65 ya Mkongoro – Chankere – Mwamgongo – Kagunga ya Chankere ambayo inapita kwenye njia ya Bonde la Ufa la Afrika Mashariki na iliyohitaji utaalamu na gharama kubwa kuijenga. Barabara hiyo imejengwa kwa kutumia fedha za Mfuko wa Barabara.